Wednesday, June 5, 2013

VIKAO VYA SINODI VYAANZA


Baada ya uzinduzi rasmi wa Sinodi katika Dominika ya Pentekoste, 19 Mei 2013, awamu ya kwanza ya vikao vya Sinodi yaanza. Awamu hii inajumuisha vikao vinavyofanyika kwa siku tano kuanzia tarehe 03 Juni hadi 07 Juni. Vikao hivi vinafanyika katika kituo cha Jimbo cha Sala na Mafungo, Epheta.

Sunday, May 26, 2013

SINODI YA JIMBO YAZINDULIWA


Kote ulimwenguni, tarehe 19 Mei Kanisa liliadhimisha Sherehe ya Pentekoste. Kwa wanajimbo la Musoma, siku hii ilikuwa na upekee zaidi. Ilikuwa ni siku ya Uzinduzi Rasmi wa Sinodi ya Jimbo. Uzinduzi huo ulifanyika kwa adhimisho la Misa Takatifu iliyoongozwa na Askofu wa Jimbo, Mhashamu Askofu Michael Msonganzila na kuhudhuriwa kwa wingi na Mapadre, Watawa na Waamini toka pembe zote za Jimbo.

Adhimisho la Misa Takatifu lililoanza majira ya saa 4:00 asubuhi, lilifanyika katika Viwanja vya Matumaini Katika Vijana, viwanja vinavyopakana na Kanisa Kuu la Jimbo. Hii ilikuwa ni Misa pekee iliyoadhimishwa kwa Jimbo zimasiku hiyo ili kuwapa nafasi mapadre wote, watawa na waamini jimboni kushiriki pamoja katika tukio hilo muhimu sana katika historia ya Jimbo. Watu walianza kukusanyika viwanjani hapo kuanzia saa moja asubuhi na kufikia majira ya saa tatu sehemu kubwa ya viwanja hivyo ilikuwa tayari imeshafurika watu. Wengi walifika kivikundi: kiparokia na vyama vya kitume wakiwa na sare zao.

Maandamano yalitanguliwa na tukio la Baba Askofu kugonga kengele ya Kanisa Kuu la Jimbo. Tendo hili lilimaanisha kuwa yeye akiwa mchungaji mkuu wa Jimbo anaitisha kusanyiko la Kijimbo kwa ajili ya kuadhimisha Sinodi na anawaalika kondoo wake kushiriki. Kisha maandamano yalianza kuelekea eneo la Ibada, eneo lililopampwa kifani kwa rangi nyekundu na nyeupe kuakisi sherehe ya Kiliturjia ya Pentekoste iliyoadhimishwa siku hiyo.

Mwanzoni mwa Misa, Pd. Robert Luvakubandi, Paroko wa Parokia ya Musoma Mjini alipata nafasi ya kutoa neno la utangulizi na kumkaribisha Baba Askofu kuongoza adhimisho. Katika neno lake, Pd. Luvakubandi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Sinodi alimjulisha Baba Askofu kuwa shughuli nzima ya maandalizi imekamilika. “Shughuli hiyo imechukua takribani miezi kumi tangu Julai mwaka jana ulipounda Kamati Kuu ya Maandalizi ya Sinodi” alieleza Pd. Luvakubandi. Alifafanua kuwa maandalizi hayo yalijumuisha vikao vya Kamati kupanga ratiba na picha nzima Maadhimisho yatakavyokuwa, kukusanya maoni toka kwa wanajimbo, kuandaa Sala ya Sinodi, kuandaa Kauli Mbiu na wajumbe wa vikao. “Maandalizi hayo” aliendelea kufafanua “yalijumlisha pia semina elekezi iliyotolewa tarehe 21 na 22 Januari kwa wajumbe wote wa sinodi uliowaalika wewe Baba Askofu”.

Katika adhimisho hilo la Misa, lililofanyika kwa uchangamfu na ushiriki hai wa waamini wote katika nyimbo na matendo mengine ya kiibada, Baba Askofu aliwaapisha wajumbe wote wa vikao vya Sinodi waliokuwapo. Wajumbe hawa ni Mapadre wote wanaofanya utume Jimboni Musoma, wawakilishi wa mashirika ya Kitawa yaliyoko Jimboni na wawakilishi kutoka parokia na taasisi zote za Jimbo. Kiapo walichokula, kwa sehemu kubwa, kilikuwa ni ungamo la Imani. Hii ni kwa sababu maadhimisho ya Sinodi ni tendo la Imani na kwa namna ya pekee yanafanyika katika Mwaka wa Imani.

Mahubiri ya Baba Askofu katika yaligusa dhamira zote za siku hiyo, yaani Sherehe ya Pentekoste, Sikukuu ya Walei na Uzinduzi wa Sinodi. “Wapendwa wanafamilia ya Mungu wa Jimbo la Musoma” ndivyo alivyoanza Baba Askofu na kuendelea “leo ni Sherehe ya Pentekoste; sherehe ambayo inahitimisha Kipindi cha Pasaka… Kwa namna ya pekee leo tunasherehekea utimilifu wa Ahadi ya Bwana Yesu kwa Mitume kabla ya kupaa kwake mbinguni, yaani ujio wa Roho Mtakatifu. Pia tunakumbuka kuzaliwa kwa Kanisa na mwanzo wa Utume wa Kanisa. Siku hii pia imewekwa na Kanisa kama sherehe ya Waamini walei”.

Baba Askofu alieleza kuwa kwa wanajimbo la Musoma kusanyiko kubwa la wanajimbo katika Sherehe hii katika Viwanja vya Matumaini katika Vijana lina umuhimu wa kipekee katika historia ya Jimbo kwa sababu ni kusanyiko pia la Uzinduzi wa Sinodi. “Kwa sababu hii twaweza kupaita mahala hapa Viwanja vya Matumaini katika Sinodi!”

Masomo ya liturjia ya siku yalitoka Mdo. 2:1 – 11; 1Kor. 12:3b – 7, 12 – 13; na Yn. 20:19 – 23. Akifanua masomo hayo, Baba Askofu alieleza kuwa Roho Mtakatifu waliyempokea Mitume, aliwapa ujasiri mkubwa wa kulihubiri Neno la Mungu. Roho huyo alikuwa ndio sababu ya Umoja na Uelewano uliokuwa umepotea kati ya Mataifa kwa sababu ya dhambi.

Aliendelea na kusema kuwa Roho Mtakatifu ndiye msingi wa karama na huduma mbalimbali katika Kanisa na ndiye anayefanya karama hizo zilete faida na umoja katika Kanisa. Aliongeza kuwa Roho huyu aliyefanya kazi ya kuwaunganisha mitume na Yesu, sasa anawaunganisha watu na Mungu kwa kuwaondolea dhambi zao. Na matunda yake makuu ni Amani kati ya Mungu na watu.

“Roho huyu tunayempokea katika maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa” alisisitiza “anatuwajibisha tumshuhudie kwa maneno na maisha yetu”. Alionya kuwa “Tunapomtambua Roho Mtakatifu kati yetu, tunalazimika tusiwe na Majivuno na Dharau kwa wengine. Roho tuliyepewa si kwa ajili ya utukufu wetu wenyewe bali ni kwa ajili ya kuujenga mwili wa Yesu yaani Kanisa”

Katika mahubiri hayo Baba Askofu aliwaalika waamini wote kumpa Roho Mtakatifu nafasi katika maisha yao ili atende kazi ndani yao. “Jenga mazingira ya Roho Mtakatifu kutenda kazi ndani yako” alisisitiza.

Baba Askofu alihitimisha mahubiri yake kwa kueleza ratiba na mada kuu za Vikao vya Sinodi. Mintarafu ratiba, alieleza kuwa maadhimisho yote ya Sinodi yanategemea kuchukua takribani Miaka Miwili hadi kuhitimishwa kwake tarehe 03 Oktoba 2014. Na ndani ya kipindi hicho matukio makuu yafuatayo yataadhimishwa. Baada ya Uzinduzi kutakuwa na vikao vikuu vine. Kikao cha Kwanza (03 – 07 Juni 2013), kikao cha Pili (09 – 13 Desemba 2013), kikao cha Tatu (28 Aprili – 02 Mei 2014) na kikao cha nne           (04 – 08 Agosti 2014).

Mada kuu zitakazojadiliwa ni mosi; UINJILISHAJI WA IMANI NA CHANGAMOTO ZA NYAKATI ZETU, MIITO NA CHANGAMOTO ZA WAKATI, pili; LITURJIA YA KANISA NA MAISHA YA SAKRAMENTI, tatu; UTUME WA HAKI, AMANI NA UPATANISHO na nne; MAENDELEO NA KUJITEGEMEA. Kisha hayo Baba Askofu alitoa tamko kuwa Sinodi Imezinduliwa.

Ilikuwa ni siku nzuri na iliyosubiriwa hamu sana na wanajimbo wote. Ikizingatiwa kuwa hii ndiyo Sinodi ya Kwanza ya Jimbo wengi wana hamasa ya kuwa washiriki katika tukio hili kubwa la kihistoria katika Jimbo. Kote jimboni sasa salamu inayotawala ni: Sinodi Musoma: Imani na Matendo, ndiyo salamu ya Sinodi.

Baadhi ya waamini waliopata nafasi ya kuzungumza na mwandishi wa makala hii hawakusita kuonesha hisia zao za furaha na matumaini makubwa kuwa adhimisho la Sinodi litafanikiwa kuliongezea jimbo uhai na ustawi.

SINODI MUSOMA: IMANI NA MATENDO.

Wednesday, May 15, 2013

VITENGE VYA SINODI VYAANDALIWA


Zikiwa zimesalia siku chache kufikia siku ya Uzinduzi wa Sinodi hapo Jumapili Mei 19, 2013, zoezi la kuandaa vitenge vya Sinodi limekamilika. Vitenge hivi vinategemewa kuwa sehemu ya vazi rasmi katika kipindi chote cha Sinodi na kubaki kama kumbukumbu ya tukio hili hata baada ya Sinodi mwisho wa mwaka 2014. Alama zilizopo kwenye kitenge hicho ni pamoja na Nembo ya Mwaka wa Imani, kauli mbiu ya Sinodi (Imani na Matendo) na mchoro wa samaki ambao ni mojawapo wa vielelezo asilia vya mkoa wa Mara lililoko Jimbo la Musoma.

Vitenge hivyo vimetengenezwa na Shirika la Masista wa Moyo Safi wa Maria Afrika, taasisi iliyokabidhiwa jukumu hilo na Kamati Kuu ya Maandalizi ya Sinodi. Akizungumza wakati wa kuvionesha vitenge hivyo mapema leo, Mama Mkuu wa Shirika hilo Sr. Lucy Magumba alieleza kuwa vitenge hivyo vimeandaliwa kwa ubora wa hali ya juu na kwa kuzingatia vionjo vya watumiaji. “Kitenge ni kipana na chenye uzito unaofaa kabisa…. Rangi ni nzuri kabisa na tumeandaa kwa rangi tatu tofauti ili kila mmoja achague rangi anayopendelea zaidi” alieleza Mama Mkuu huyo na kuongeza kuwa kutokana na ubora wake watu waweza kushona mashati au makoti hasa kwa akinababa na aina nyinginezo za mavazi kwa akinamama.
Sr. Lucy Magumba, Mama Mkuu IHSA akionesha sampuli ya vitenge vya Sinodi

Vitenge vitapatikana katika kipindi chote cha Sinodi. Wakazi wa Musoma waweza kununua vitenge hivyo kutoka katika duka la vitabu la Jimbo lililoko jengo la RC Conference Centre. Walio nje ya Musoma na wengineo waweza kuagiza kutoka Makao Makuu ya Shirika IHSA. Kwa mawasiliano: Sr. Stella Matutina 0752 225 771.


Friday, May 10, 2013

MAANDALIZI YA UFUNGUZI YAPAMBA MOTO

Kuelekea tukio la ufunguzi wa Sinodi ya Jimbo la Musoma, maandalizi yazidi kupamba moto ili tukio hilo liweze kufana. Waamini kote Jimboni wanasubiri kwa hamu tukio hilo la kihistoria na lenye umuhimu wa pekee katika maisha na ustawi wa Jimbo.

Akielezea maandalizi hayo mapema leo, Mwenyekiti wa Kamati Kuu ya Sinodi, Mhe. Pd. Robert Luvakubandi alisema kuwa tayari Baba Askofu ameshatoa barua ya kutangaza ufunguzi rasmi wa Sinodi. Ufunguzi huo utafanyika siku ya Pentekoste tarehe 19 Mei mwaka huu 2013 katika viwanja vya Matumaini Katika Vijana. “Maelekezo maalumu pia yametolewa kwa maparoko kuwaandaa waamini kushiriki kikamilifu katika tukio hili” aliongeza Pd. Luvakubandi ambaye pia ni Paroko wa Parokia ya Musoma Mjini.

Aidha, Pd. Luvakubandi aliainisha kamati mbalimbali zilizoundwa kuandaa na kutoa huduma mbalimbali siku hiyo. Nazo ni Kamati ya Liturjia chini ya uenyekiti wa Pd. Benedict Luzangi, Kamati ya Usafi wa Mazingira, Jukwaa, Maturubai na Viti chini ya Uenyekiti wa Pd. Jeremiah Musira na Kamati ya Chakula na Vinywaji chini ya Uenyekiti wa Pd. Julius Magere.

Nyingine ni Kamati ya Afya chini ya Sr. Anastazia Salla CDNK na Sr. Bernadeta Beda IHSA, Kamati ya Fedha chini ya Pd. Leo Kazeri na Kamati ya Ulizi chini ya Nd. Egid Kilosa.

Kamati ya Liturjia itawajumuisha pia Sr. Winifrida Nyafuru IHSA (Katibu) na wajumbe Mnovisi Elizabeti Saka, Mnovisi Yasinta Cosmas, Shemasi William Bahitwa, Kat. Fredrik Raymond na Kat.Thomas Shagga. Wajumbe wengine wa kamati hii ni Mwl. Sospeter Chacha, Ms. Regina, Stella Dunia, Generose Mujuni na Mrs. Lucas Hupa.

Katibu wa kamati ya Usafi, Jukwaa, Maturubai na Viti ametajwa kuwa ni Br. Masini Kaswamila. Wajumbe wa Kamati hiyo ni Pd. Pius Msereti, Victor Mujuni, Maria Aloyce na Deogratias Nyantira.

Kamati ya Chakula na Vinywaji itawajumuisha Sr. Rose Aloyse (Katibu) na wajumbe Ma. Restituta Lukona, Monica James, Mwl. Maryness Martine na Nd. John Mkombozi.

Ms. Liz Mach na Nd. Archard Rwamunwa watakuwa katika Kamati ya Fedha watakaosaidia katika Ulinzi ni VIWAWA Parokia ya Musoma Mjini na Jeshi la Polisi.

Wahusika wote hawa wameombwa kukutana na Mwenyekiti wa Kamati Kuu pamoja na Sekretarieti ya Sinodi siku ya Jumatatu Mei 13. “Nimewaalika tukutane Kanisa Kuu katika Bustani ya Mwenyeheri Yohane Paulo II saa 10 Jioni” alisema Pd. Luvakubandi.

Ni matumaini ya kila mwenye mapenzi mema na Jimbo la Musoma kuwa Ufunguzi wa Sinodi utaashiria mwanzo wa kipindi cha pekee cha neema katika Jimbo.

Wednesday, May 8, 2013

UFUNGUZI RASMI WA SINODI YA JIMBO

Mh. Baba Askofu Michael Msonganzila ametoa barua ya kutangaza ufunguzi rasmi wa Sinodi ya Jimbo. Barua hiyo iliyotolewa tarehe 5 Mei 2013 imethibitisha kuwa ufunguzi huo utafanyika siku ya Pentekoste tarehe 19 Mei 2013. “Misa itafanyika katika makao makuu ya Jimbo, yaani Parokiani Musoma Mjini katika viwanja vya Matumaini katika Vijana kuanzia saa 4:00 asubuhi. Misa itaongozwa nami Mhashamu Baba Askofu Michael Msonganzila”, ilieleza sehemu ya barua hiyo.

Itakumbukwa kuwa ni katika viwanja hivyo Baba Askofu alitangaza kwa mara ya kwanza nia ya kuitisha Sinodi ya Jimbo. Tangazo hilo alilitoa tarehe 3 Oktoba 2011 katika maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 100 ya Ukristo Jimboni. Viwanja hivyo vitawapokea tena waamini kutoka kila pembe ya Jimbo letu katika tukio kubwa la ufunguzi wa Sinodi wiki mbili zijazo.

Katika barua hiyo Baba Askofu alieleza pia kuwa ndani ya adhimisho la Misa ya ufunguzi atawaapisha wawakilishi wote aliowateua kushiriki mikutano mikubwa ya Sinodi. Wawakilishi hao “wataapishwa kwa sababu tendo la maadhimisho ya Sinodi ni tendo la Imani Katoliki”, alieleza.

Siku hiyo kutakuwa na Misa Moja tu katika Jimbo zima. Kwingineko maparokiani, hasa parokia zilizo nje ya udekano wa Musoma Mjini, ruhusa ya pekee imetolewa kwa Mapadre kusali Misa ya Kesha la Pentekoste Jumamosi jioni tarehe 18 Mei. Watashiriki Misa ya kesha hasa wale ambao hawatapata bahati ya kushiriki Misa ya Jumapili ya Pentekoste Musoma. Aidha, Makatekista wataongoza Ibada ya Dominika bila Padre siku ya Jumapili kwa wale ambao hawakushiriki Misa ya Kesha.

“Nawatakia maandalizi mema ya matukio hayo muhimu yaliyoko mbele yetu yanayogusa uhai na ustawi wa Jimbo letu la Musoma” alihitimisha Baba Askofu.

Tuesday, March 5, 2013

Sinodi katika Historia ya Kanisa (Pd. Laurenti Magesa)

Pd. Laurenti C. Magesa alikuwa ni mmojawapo wa wawezeshaji katika semina elekezi ya Sinodi ya Jimbo. Katika semina hiyo, alitoa mada kuhusu Sinodi katika Historia ya Kanisa.

Ifuatayo ni mada aliyoitoa kama ilivyokaririwa na Sekretarieti ya Kamati Kuu ya Maandalizi ya Sinodi.

SEMINA ELEKEZI YA SINODI YA JIMBO

Tarehe 21 na 22 Januari 2013 ilifanyika semina elekezi ya Sinodi ya Jimbo katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Mwembeni. Wawezeshaji katika semina hiyo walikuwa ni Pd. Romuald Kajara wa Jimbo la Rulenge - Ngara na Pd. Laurenti Magesa wa Jimbo la Musoma.

Ifuatayo ni hotuba iliyotolewa na Mhashamu Baba Askofu Michael Msonganzila wakati wa ufunguzi wa semina hiyo. Hotuba ya Baba Askofu ilieleza maana na malengo ya sinodi kwa ujumla pamoja na sababu za kuadhimisha sinodi katika jimbo la Musoma.

Thursday, November 1, 2012

SABABU ZA KUADHIMISHA SINODI JIMBONI MUSOMA

Wapendwa wanafamilia ya Mungu, katika kikao cha kwanza cha kamati kuu ya maandalizi ya Sinodi, Baba Askofu Michael Msonganzila aliweka wazi sababu tisa zinazotufanya tuadhimishe Sinodi wakati huu. Tunapenda sasa wasomaji wetu wapendwa wazifahamu sababu hizi muhimu kwetu katika kuadhimisha Sinodi ya Jimbo letu la Musoma.

Wednesday, September 5, 2012

Takwimu za Jimbo la Musoma

Endapo unapenda kuzifahamu takwimu muhimu za Jimbo la Musoma, uitembelee tovuti ya Catholic Hierarchy inayokusanya takwimu zote za Maaskofu na Majimbo ya dunia nzima. Ukurasa unaohusu Jimbo letu la Musoma unapatikana hapa. Katika ukurasa huo utapata habari za historia ya Jimbo, taarifa za Maaskofu wote walioongoza Jimbo letu, takwimu za waamini, anuani na kadhalika. Ifahamu Jimbo lako la Musoma!

Sehemu ya ukurasa wa Jimbo la Musoma
katika tovuti ya Catholic Hierarchy

Moyo wa Jimbo la Musoma

Mahali Jimbo la Musoma lilipozaliwa
mnamo tarehe 3 Oktoba 1957 - siku Askofu wa kwanza wa Jimbo,
Mhashamu John James Rudin, alipowekwa wakfu kuwa Askofu
Patakatifu pa Kanisa Kuu la Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, Musoma mjini
Altare ya Somo wa Kanisa Kuu na Jimbo - Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu
Tabernakulo ya Kanisa Kuu la Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, Musoma mjini